Ruka hadi Yaliyomo
AfroCave

Kifungu 24. Mipaka ya Haki au Uhuru wa Kimsingi

(1) Haki ya uhuru wa kimsingi iliyo katika Sheria ya Haki haiwezi kuwekewa mipaka isipokuwa kupitia kwa sheria na iwe tu kwamba mipaka ina maana, na ni ya haki katika jamii iliyo wazi na ya kidemokrasia, na chini ya misingi ya heshima ya binandamu, usawa na uhuru, na kwa kuzingatia vipengele muhimu vikiwemo–

  • (a) hali ya haki hiyo au uhuru wa kimsingi;
  • (b) umuhimu wa lengo la mipaka hiyo;
  • (c) hali na kiwango cha mipaka hiyo;
  • (d) haja ya kuhakikisha kuwa kufurahia wa haki hizo na uhuru huo wa kibinafsi kwa mtu yeyote hautatizi haki na uhuru wa kimsingi wa watu wengine; na
  • (e) uhusiano uliopo kati ya mpaka na lengo lake na endapo kuna njia zingine zisizotatiza za kufikia lengo hilo.

(2) Licha ya ibara ya (2), sharti la sheria linalowekea mipaka haki au uhuru wa kimsingi–

  • (a) ikiwa ni sharti lililotungwa au kurekebishwa kabla au baada ya siku ya kuanza kutumika Katiba hii, si halali, isipokuwa sheria hiyo haswa inadhihirisha madhumuni ya kuiwekea mipaka haki hiyo au uhuru wa kimsingi na kiwango cha mipaka hiyo;
  • (b) halitachukuliwa kama kuzuia haki au uhuru uliotajwa katika Sheria ya Haki isipokuwa pale ambapo sharti hilo linaeleza wazi na kwa yakini kuhusu haki au uhuru wa kimsingi unaopaswa kuzuiwa na hali au kiwango cha mipaka hiyo; na
  • (c) halitazuia haki au uhuru wa kimsingi unaotajwa katika Sheria ya Haki ili kupunguza uzito na umuhimu uliowekwa katika haki hiyo.

(3) Serikali au mtu anayetaka kuhalalisha mpaka fulani atapaswa kuthibitishia mahakama, mahakama maalum au mamlaka nyingine kuwa mahitaji ya Kifungu hiki yameridhishwa.

(4) Masharti katika Sura hii kuhusu usawa yatatumika kwa wote ila tu pale ambapo patahitajika utekelezaji wa Sheria ya Kiislamu mbele ya mahakama za Kadhi kwa waumini wa Kiislamu kwa mujibu wa hadhi zao za kibinafsi, hali ya ndoa, talaka na urithi.

(5) Licha ya ibara za (1) na (2), sharti la sheria linaweza kuwekea mipaka utekelezaji wa haki na/au uhuru wa kimsingi katika masharti kwa watu wanaohudumu katika Vikosi vya Usalama vya Kenya, au Huduma za Polisi za Kitaifa–

  • (a) Kifungu cha 31- Faragha;
  • (b) Kifungu cha 36 -Uhuru wa kutangamana
  • (c) Kifungu cha 37- Mikutano, maandamano, migomo na malalamiko;
  • (d) Kifungu cha 41 –Mahusiano ya kikazi;
  • (e) Kifungu cha 43 – Haki za kiuchumi na kijamii;
  • (f) Kifungu cha 49 –Haki za watu waliotiwa mbaroni;