Ruka hadi Yaliyomo
AfroCave

Kifungu 22. Utekelezaji wa Sheria ya Haki

(1) Kila mtu ana haki ya kuwasilisha kesi mahakamani akidai kunyimwa, kukiukwa, au kutishiwa haki au uhuru wa kimsingi ulioko katika Sheria ya Haki.

(2) Pamoja na kuwasilishwa na mtu anayewawakilisha, kesi chini ya ibara ya (1) inaweza kuwasilishwa mahakamani na–

  • (a) mtu anayemwakilisha mtu mwingine asiyeweza kujiwakilisha;
  • (b) mtu ambaye pia ni mwanachama wa kundi fulani au kwa hiari ya kundi au tabaka fulani la watu;
  • (c) mtu aliyejitolea kwa niaba ya umma; na
  • (d) muungano uliojitolea kwa niaba ya mtu mmoja au kundi miongoni mwa wanachama.

(3) Jaji Mkuu ataweka kanuni zinazoruhusu kesi zilizotajwa katika kifungu hiki ambazo zitaridhisha kigezo kwamba–

  • (a) haki za kulalamika zilizotolewa katika ibara ya (2) zinatekelezwa kwa ukamilifu;
  • (b) urasmi unaohusiana na kesi hizo, kukiwemo kuanzishwa kwa kesi, unawekwa kwa kiwango cha chini, na hasa pakiwa na haja, mahakama itakubali kuwepo kwa kesi kwa misingi ya rekodi zisizo na ulazima wa urasmi;
  • (c) hakuna fedha zitakazotozwa kwa kuanzisha kesi;
  • (d) mahakama, kwa kuzingatia kanuni za haki za kimsingi haitazuiwa bila sababu na mahitaji madogo madogo; na
  • (e) shirika au mtu binafsi mwenye ujuzi maalum anaweza, kwa idhini ya mahakama, kujitokeza kama rafiki wa mahakama.

(4) Kukosekana kwa kanuni zinazoangaziwa katika ibara ya (3) hakutamnyima yeyote haki ya kuwasilisha malalamiko kulingana na Kifungu hiki, kusikizwa kwa malalamiko hayo na kuamriwa na mahakama.