Ruka hadi Yaliyomo
AfroCave

Kifungu 95. Majukumu ya Baraza la Kitaifa

(1) Baraza la Kitaifa linawakilisha watu wa maeneobunge na walio na maslahi maalumu katika Baraza la Kitaifa.

(2) Baraza la Kitaifa hushauriana kuhusu na kusuluhisha masuala yenye umuhimu mkubwa kwa watu.

(3) Baraza la Kitaifa linatunga sheria kwa kuzingatia Sehemu ya 4 ya Sura hii.

(4) Baraza la Kitaifa–

  • (a) hubainisha ugavi wa mapato ya kitaifa kati ya ngazi za Serikali, kama inavyoagizwa katika Sehemu ya 4 ya Sura ya Kumi na Mbili;
  • (b) hugawa hazina ya fedha kwa matumizi ya Serikali ya kitaifa na asasi nyingine za Serikali ya kitaifa; na
  • (c) hutekeleza usimamizi wa jumla wa mapato ya kitaifa pamoja na matumizi yake.

(5) Baraza la Kitaifa–

  • (a) linachunguza utendakazi wa Rais afisini, Naibu wa rais na maafisa wengine wa Serikali na ikiwezekana kuchukua hatua za kuwatoa afisini; na
  • (b) litasimamia asasi za Serikali;

(6) Baraza la Kitaifa litaidhinisha tangazo la vita na kutathmini ongezeko la hali ya hatari nchini.