Ruka hadi Yaliyomo
AfroCave

Kifungu 261. Sheria Zinazohusiana na Matokeo

(1) Bunge litatunga sheria yoyote inayohitajiwa na Katiba hii, itungwe ili kushughulikia jambo fulani katika muda ulioelezwa katika Mpangilio wa Tano, kuanzia tarehe ya kutekelezwa kwa Katiba hii.

(2) Licha ya ibara ya (1), Baraza Kuu la Kitaifa linaweza, kupitia kwa uamuzi utakaoungwa mkono na idadi ya kura isiyopungua thuluthi mbili ya Wabunge wote, Baraza Kuu la Kitaifa linaweza kuongeza muda uliowekwa kuhusiana na suala lolote kama inavyoelezwa katika ibara ya (1), kwa muda usiozidi mwaka mmoja.

(3) Uwezo wa Baraza la Kitaifa kama ulivyoelezwa katika ibara ya (2) unaweza kutumika–

  • (a) Mara moja tu kuhusiana na suala fulani; na
  • (b) Katika hali maalum ambayo itaidhinishwa na Spika wa Baraza la Kitaifa.

(4) Kwa sababu ya ibara ya (1), Mwanasheria Mkuu akishauriana na Tume ya Utekelezaji wa Katiba hii, atatayarisha na kuwasilisha Miswada Bungeni, kwa haraka inavyowezekana, ili kuwezesha Bunge kupitisha sheria katika muda uliowekwa.

(5) Kama Bunge litashindwa kupitisha sheria yoyote kwa kipindi kilichowekwa, mtu yeyote anaweza kupeleka malalamiko kwa Mahakama ya Juu kuhusiana na jambo hilo.

(6) Katika kuamua juu ya malalamiko hayo chini ya ibara ya (5) , Mahakama ya Juu inaweza–

  • (a) Kutoa agizo kuhusu jambo hilo; na
  • (b) Kuelekeza agizo hilo kwa Bunge na Mwanasheria Mkuu ili kuchukua hatua za kuhakikisha kwamba sheria inayohitajika imepitishwa katika muda uliowekwa katika agizo hilo, na kutoa ripoti kuhusu utekelezaji huo kwa Jaji Mkuu.

(7) Iwapo Bunge litashindwa kuunda sheria kulingana na agizo chini ya ibara ya (6) (b), Mwanasheria Mkuu atamshauri Rais kuvunja Bunge na Rais atalivunja Bunge.

(8) Iwapo Bunge limevunjwa chini ya ibara ya (7), Bunge jipya litaunda sheria hiyo inayohitajika katika muda uliolezwa katika Mpangilio wa Tano, kuanzia tarehe ya kuanza kwa kipindi cha Bunge jipya.

(9) Ikiwa Bunge jipya litashindwa kuunda sheria kulingana na ibara ya (8), masharti ya ibara ya (1) hadi ya (8) yatatekelezwa upya.