Ruka hadi Yaliyomo
AfroCave

Kifungu 216. Majukumu ya Tume ya Ugavi wa Mapato

(1) Jukumu kuu la Tume ya Ugavi wa Mapato ni kutoa mapendekezo kuhusu ugavi unaozingatia usawa wa mapato yanayozalishwa na serikali ya kitaifa–

  • (a) kati ya serikali ya kitaifa na serikali za kaunti; na
  • (b) miongoni mwa serikali za kaunti.

(2) Tume hii pia itatoa mapendekezo kuhusu ufadhili wa serikali za kaunti na usimamizi wa fedha katika serikali hizi; kwa mujibu wa Katiba hii na sheria za kitaifa.

(3) Katika kutoa mapendekezo, Tume hii itahitaji–

  • (a) kuinua na kudumisha kigezo kilichotajwa katika kifungu cha 203 (1);
  • (b) kwa wakati mwafaka, kueleza na kuwezesha njia za kuzalisha mapato za serikali ya kitaifa na serikali za kaunti; na
  • (c) kuhimiza uwajibikaji wa kifedha.

(4) Tume itaamua, kuchapisha na kuchunguza kila mara sera ambayo itatoa kigezo cha kutambua maeneo yaliyotengwa katika kifungu cha 204 (2).

(5) Tume itawasilisha mapendekezo yake kwa Seneti, Baraza la Kitaifa, Serikali ya kitaifa, mabaraza ya kaunti na kamati kuu ya Kaunti.