Ruka hadi Yaliyomo
AfroCave

20. Tume ya Huduma za Mahakama

(1) Tume ya Huduma za Mahakama itateuliwa katika siku sitini baada ya tarehe ya kutekelezwa kwa Katiba hii, na Tume hii itachukuliwa kuwa imeundwa chini ya Katiba hii licha ya kwamba huenda kukawa na nafasi wazi katika uanachama wake kwa kuwa idara yoyote inayowateua au kuwachagua wanachama haitakuwa imefanya hivyo.

(2) Licha ya ibara ndogo ya (1), Tume ya Huduma za Mahakama haitatekeleza majukumu yake hadi wanachama wasiopungua watano wawe wameteuliwa.

(3) Ili kuhakikisha kuna mwendelezo katika shughuli za Tume ya Huduma za Mahakama, licha ya Kifungu cha 171 (4), wakati Tume itakapoundwa kwa mara ya kwanza, wanachama wafuatao watateuliwa kuhudumu kwa miaka mitatu pekee–

  • (a) Jaji wa Mahakama ya Rufani atakayeteuliwa chini ya Kifungu cha 171 (4) (c);
  • (b) Jaji wa Mahakama ya Juu atakayeteuliwa chini ya Kifungu cha 171 (4) (d);
  • (c) Mmoja wa mawakili atakayeteuliwa chini ya Kifungu cha 171 (4) (f), atakayeteuliwa na idara inayosimamia shughuli za taaluma ya mawakili; na
  • (d) mmoja wa wanachama atakayeteuliwa na Rais chini ya Kifungu cha 171 (4) (h); atakayetambuliwa na Rais.

(4) Hadi Tume ya Huduma za Umma inayorejelewa katika Kifungu cha 233 itakapoundwa, mtu anayeteuliwa na Tume ya Huduma za Umma chini ya ibara ya 106 ya Katiba ya awali atahudumu katika Tume ya Huduma za Mahakama lakini, wakati Tume mpya ya Huduma za Umma itakapoundwa, mtu huyo ataacha kuwa mwanachama wa Tume ya Huduma za Mahakama na Tume hiyo mpya ya Huduma za Umma itamteua mtu atakayehudumu katika Tume ya Huduma za Mahakama.